test

Ijumaa, 4 Mei 2018

Serikali Kutaifisha Pamba Itakayonunuliwa Nje Ya Mfumo Wa Vyama Vya Ushirika Vya Msingi


Na Stella Kalinga, Simiyu
Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Pamba nchini Marco Mtunga amewaonya wanunuzi wa Pamba watakaonunua pamba nje ya mfumo wa Vyama vya Ushirika vya Msingi (AMCOS) na kuwa endapo watabainika Pamba hiyo itataifishwa na Serikali.

Onyo hilo limetolewa Mkoani Simiyu katika kikao baina ya Viongozi wa mkoa huo, viongozi wa vyama vya ushirika vya Msingi (AMCOS), wanunuzi wa Pamba na Naibu Mrajisi  kutoka Tume ya Maendeleo ya Ushirika Dodoma Charles Malunde, lengo likiwa ni kukumbusha juu ya uadilifu katika masuala ya ununuzi wa pamba, ikiwa ni maandalizi wa ununuzi pamba baada ya msimu kufunguliwa.

Mtunga amesema mwaka huu Serikali imefanya uamuzi kwamba pamba yote itakayozalishwa hapa nchini itanunuliwa kupitia Vyama vya Msingi (AMCOS) jambo ambalo amesema limeelezwa vizuri katika mwongozo wa bodi.

“Tunawatahadharisha wanunuzi wa pamba kufuata mfumo wa ununuzi wa pamba uliowekwa na Serikali, pamba yote itakayokamatwa ikiwa haikununuliwa kupitia Chama cha Ushirika cha Msingi itataifishwa na Serikali,  katika mwongozo tulioutoa maelekezo hayo yapo na yako chini ya sheria Namba 2 ya pamba ya mwaka 2001” alisema Mtunga.

Kwa upande wake Naibu Mrajisi kutoka Tume ya Maendeleo ya Ushirika Dodoma Charles Malunde amewataka viongozi wa Vyama vya ushirika kuepuka aina yoyote ya wizi na ubadhilifu wa kutumia udanganyifu wa kuwaibia wakulima kwa kuziharibu mizania.

Aidha, Malunde amesisitiza sheria na taratibu za Ushirika zizingatiwe katika uendeshaji wa Vyama vya Ushirika vya Msingi, hivyo akawataka viongozi wote waliochaguliwa kuongoza vyama hivyo ambao wana shutuma zozote, watumishi wa Umma au Viongozi wa Serikali na Vyama vya Siasa kuachia mara moja nafasi hizo kwa kuwa hawana sifa kwa mujibu wa sheria.

Baadhi ya viongozi wa AMCOS waliwasilisha masuala mbalimbali kama maombi yao kwa Serikali kuhusiana na ununuzi wa pamba ikiwa ni pamoja na kuomba vyama vya ushirika vya msingi vipya vilivyo  katika hatua ya usajili vikamilishiwe usajili ili viweze kuingia katika mfumo huu wa ununuzi wa pamba.

Akihitimisha kikao hicho Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Anthony Mtaka amesema anatamani kuona ushirika wenye mtazamo wa kujibu changamoto na mahitaji ya wakulima wa pamba, huku akitoa angalizo kwa viongozi wa AMCOS watakaofanya ubadhilifu wa fedha za Vyama vya Ushirika kuwa Serikali mkoani humo itawachukulia hatua kali.

“Ushirika wa Simiyu (is my own baby) ni mtoto wangu mwenyewe, ni kitu ambacho nilitamani kuona kinatokea, Wanaushirika wakakaokosa uadilifu wajihesabu kuwa wafungwa watarajiwa, nawaambia nitawafunga na sitanii nitawafunga” alisisitiza Mtaka.

Katika hatua nyingine amemtaka Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi kuaandaa eneo la ujenzi wa Makao Makuu ya Chama Kikuu cha Ushirika Simiyu.

Install Application ya JUNGUKUULEO Uweze Pata Habari Kirahisi Zaidi

xxxxxxxxxxxxx

0 comments:

Chapisha Maoni