WAFANYAKAZI
wanane wa kiwanda cha nondo cha Bansal kilichopo Kisongo wilayani
Arumeru, Arusha, wameungua sehemu mbalimbali za miili yao baada ya uji
wa chuma uliokuwa ukichemka kuwarukia.Tukio hilo lilitokea jana
kiwandani hapo na kuwasababishia wafanyakazi hao majeraha sehemu
mbalimbali za miili yao ambapo walikimbizwa Hospitali ya Selian iliyopo
jijini hapa.
Akizungumza jana
hospitalini hapo, daktari aliyewahudumia wagonjwa hao, Rose Kaaya
alisema aliwapokea majeruhi hao majira ya asubuhi kuanzia saa tatu ambao
wameumia sehemu mbalimbali za miili yao huku wengine wakishonwa nyuzi
kadhaa kwa sababu ya kuchanwa na vyuma wakati wakikimbia kujiokoa.
Dk Kaaya aliwataja
majeruhi hao kuwa ni Hassan Guni (27), Christopher Semkiwa (24), Fred
Sungi (21), Andrew Kihundwa (26), Calvin Langu (19), Simon Mkumbo (34),
Simon Njuguna (25) na Tilak Tiwakraj (34), Mtanzania mwenye asili ya
Asia.
Alisema majeruhi hao
walipokewa hospitalini hapo na kutibiwa majeraha yao mbalimbali
waliyoyapata kutokana na uji wa moto huo. Aliongeza kuwa, wameumia
sehemu mbalimbali ikiwa ni pamoja na nyuma ya shingo, mikononi na sehemu
nyingine za miili yao.
Alisema majeruhi hao
walitibiwa na kuruhusiwa kurudi nyumbani kisha kushauriwa kurudi leo
hospitalini hapo kwa ajili ya kuangaliwa kwa ukaribu maendeleo ya
vidonda vyao.
Mmoja wa majeruhi hao,
Njuguna alisema awali asubuhi waliingia kazini kama kawaida, lakini
baada ya muda waliona uji wa moto ukiruka na kuanza kuwaunguza kisha wao
kukimbia ili kujiokoa.
“Hatujui chanzo cha
kuruka kwa moto huu ila tumeungua sehemu mbalimbali za miili yetu na
tunashukuru tumepata huduma za matibabu ila tumeungua,” alieleza.