test

Alhamisi, 9 Julai 2015

Channel Ten, Star tv, TBC Zaadhibiwa na TCRA




MAMLAKA ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imetoa adhabu ya faini kwa vituo vitatu vya televisheni nchini kwa kuonyesha vipindi vilivyokiuka kanuni za huduma ya  utangazaji (maudhui ) ya mwaka2005.
 
Uamuzi huo ulitolewa jijini Dar es salaam jana  na kamati ya Maudhui ya TCRA chini ya mwenyekiti wake Mhandisi Margaret Munyagi ambapo alivitaja vituo hivyo kuwa ni Channel Ten, Star TV na TBC1.
 
Munyagi alisema ushahidi ulionyesha kuwa vituo hivyo kwa nyakati tofauti na katika vipindi tofauti walikiuka kanuni za Huduma ya utangazaji .
 
 Akizungumzia Kituo cha Channel Ten alisema kimepewa onyo kali na kutakiwa kulipa faini ya Sh Milioni 2.5, kwa kukiuka kanuni  kwa makosa mawili Mei 30 mwaka huu kupitia kipindi cha Kanjanja Time kilichorushwa hewani kuanzia 2:45 hadi 3:10 usiku ambapo walionyesha picha ya mgonjwa akiwa katika wodi ya Hospitali ya Serikali mjini Songea huku sehemu ya makalio yake yakiwa wazi na kuonyesha vidonda.
 
Alisema taarifa hiyo  ilirudiwa mara kadhaa huku watangazaji
wakisikika wakishabikia uchochezi dhidi ya serikali kwamba madaktari wafukuzwe na hospitali ifungwe
 
“Kipindi hicho pia kilionyesha taarifa ya walemavu wawili wakipigana hadharani huku watangazaji wa kipindi wakishangilia kitendo hicho na kufananisha na pambano la ngumi za kulipwa” alisema Munyagi.
 
 Alisema kituo hicho kimekiuka kanuni  namba 5(c), (h), 9(1),  18(1), (b), (i), (ii) za  huduma ya utangazaji  ya 2005 zinazotaka kituo kuhakikisha kinazingatia ubora wa vipindi pamoja na staha, ambavyo havileti uchochezi wala kujenga chuki katika jamii, kutokungilia masuala binafsi,  na kutochochea vurugu na ukatili.
 
Kwa upande wa kituo cha Televisheni ya Taifa (TBC), Munyagi alisema kimetakiwa kutoa faini ya Sh 500,000 kukiuka kanuni za huduma ya utangazaji (maudhui) 2005 namba 9(2) na 9(3) katika kipindi cha Taarifa ya Habari, Machi 21 mwaka huu kwa kuonyesha utambulisho wa mtoto aliyelawitiwa.
 
“Taarifa hiyo ilionyesha utambulisho wa picha na majina ya wazazi wa mtoto, eneo analoishi, nyumba , shule anayosoma na sehemu ya mwili wa mtoto wakati akiwa anatembea jambo ambalo ni ukiukwaji wa kanuni za huduma za utangazaji” alisema Munyagi.
 
 Alisema Kituo cha Star TV  nacho kimetakiwa kutoa faini ya Sh 500,000, kwa kukiuka kanuni za huduma za utangazaji  2005 namba 5(c), 5(g),  14(1), 16(3), 26(1) na 26(2) katika kipindi cha Min Buzz kilichorushwa hewani Juni 3 mwaka huu saa 12:30 jioni hadi 1:00 usiku na kujadili mada inayohusu ubakaji katika ndoa wakati ambao watoto pia hupata fursa ya kuangalia na kusikiliza.
 
Alisema  vituo vyote vinatakiwa kulipa faini hizo ndani ya siku 30 na pia vinahaki ya kukata rufaa dhidi ya uamu huo ambapo ni ndani ya siku 30 tangu uamuzi ulipotolewa.

Install Application ya JUNGUKUULEO Uweze Pata Habari Kirahisi Zaidi

xxxxxxxxxxxxx

0 comments:

Chapisha Maoni