test

Ijumaa, 12 Juni 2015

Kiongozi wa waasi wa ADF Aliyekamatwa Tanzania Agoma Kurudishwa Uganda




KIONGOZI wa Kundi la Kigaidi la Waasi la ADF  nchini Uganda, Jamil Mukulu amedai  hataki kurudishwa kwao kwa sababu hana imani na mahakama yoyote nchini Uganda.
 
Anadai anaamini kesi yake ikisikilizwa nchini humo hawezi kutendewa haki ni bora ikasikilizwa katika mahakama yoyote lakini si huko.
 
Mukulu  alidai hayo kwa kupitia Wakili wake Martin Rwehumbiza ambaye aliwasilisha hoja hizo jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi, Cyprian Mkeha.
 
“Mheshimiwa hakimu naomba mteja wangu asirudishwe Uganda, kesi yake isikilizwe mahali popote lakini siyo nchini Uganda, nina kila sababu ya kuamini kwamba hatatendewa haki,”alidai Rwehumbiza.
 
Alidai mteja wake kwa takribani miaka 20 amekuwa akikimbia kimbia nchini humo kutokana na utofauti aliokuwa nao na serikali ya nchi hiyo kutokana na itikadi za kisiasa hivyo ana kila sababu ya kuamini hakuna mahakama ya Uganda itakayosikiliza kesi yake na kumtendea haki.
 
Akijibu hoja hizo Wakili wa Serikali Mkuu, Edwin Kakolaki alidai upande wa Jamhuri ulidhani mshtakiwa angekana kuhusika katika mauaji kuliko kuanza kueleza kwamba anatofautiana na Serikali ya Uganda.
 
Alidai kuhusu suala la mshtakiwa kutotendewa haki  kuna barua kutoka Uganda inayomuhakikishia kuwa anakabiliwa na makosa ya mauaji na yapo kwa mujibu wa sheria na si siasa.
 
“Upande wa mashtaka hatuwezi kufanya kazi kwa dhana, hiyo barua imeihakikishia mahakama Uganda mshtakiwa atatendewa haki, mauaji hayana mahusiano na masuala ya kisiasa, naomba mahakama itilie maanani maombi yetu,”alidai.
 
Mahakama baada ya kusikiliza hoja za pande zote mbili iliahidi kutoa uamuzi wa mshtakiwa kurudishwa Uganda ama la Juni 12.
 
Awali inadaiwa mshtakiwa huyo anakabiliwa na kesi namba AA16/2015 ya mauaji ambapo anashtakiwa pamoja na wenzake kuwa kati ya Mei, 2014 na Februari 2015 katika Wilaya ya Mayuge, Namanyingo na Bugiri washtakiwa waliwaua baadhi ya watu maarufu wa Uganda.
 
Aliwataja watu hao kuwa ni Sheikh Ductoor Abduladir Mwaya, Tito Okware, Askari Polisi mwenye namba 54812 Babale Muzamir, Polisi mwenye namba 1404 SPC Kemywa Karim, Polisi namba 44957 Koplo Owol Julius, Macho Stevena na Owol John Steven.
 
Alidai watu hao waliuwawa kwa kupigwa risasi na baada ya tukio hilo Polisi wa Uganda waliwakamata washtakiwa Salim Alli Yahya, Sharif Abdallah, Mussa Mukudanchu Nabangi, Adam Amisi, Abdulmalik Kabaale na Kabalribwe Ally.
 
Waliokamatwa walikiri kuhusika na mauaji, pia walikiri kuwa ni waasi wa ADF ambalo Uganda lilihalalishwa kuwa ni kundi la kigaidi, walikubali kuua kwa maelekezo ya Mukulu ambaye ni kiongozi wa kundi hilo la waasi.

Install Application ya JUNGUKUULEO Uweze Pata Habari Kirahisi Zaidi

xxxxxxxxxxxxx

0 comments:

Chapisha Maoni