test

Jumanne, 18 Oktoba 2016

Waziri Wa Fedha Aitaka Benki Ya Maendeleo Tib Kujikita Katika Uwekezaji Wa Viwanda



Waziri wa Fedha na Mipango Dk. Philip Mpango amezindua rasmi bodi ya wakurugenzi ya Benki ya Maendeleo TIB kwa kuiagaiza iweke mikakati yakutaua changamoto mbalimbali zitakozoiwezesha kushiriki kikamilifu katika utelezaji wa Mpango wa pili wa maendeleo wa miaka mitano.
Bodi hiyo imeundwa kufuatia uteuzi wa Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli uliofanyika mwezi  Julai 2016.

Akizindua bodi hiyo, Dkt. Mpango aliwakumbusha wajumbe kufanya kazi kwa ufanisi na weledi ili kuweza kufanikisha azma ya Rais ya kujenga Tanzania ya Viwanda.
 
“Serikali ya awamu ya tano imejikita kwenye kuhakikisha kuwa uchumi wetu unakuwa ni uchumi wa viwanda. Benki hii ikiwa ni benki ya kisera inawajibu wa kuhakikisha hili linatekelezwa. Kwa mantiki hiyo ni matarajio ya serikali kuona kuwa benki inachochea maendeleo katika nyanja zote muhimu za uendelezaji wa viwanda  vya kuzalisha umeme na miundombinu yake, maji, barabara/usafirishaji na mawasiliano ili  kufikia malengo tarajiwa hususan kuhakikisha kuwa Tanzania inakuwa ni nchi ya uchumi wa kati unaotegemea viwanda ” alisema Dkt. Mpango.

Kwenye maelezo yake ya awali, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo TIB, Charles Singili mbali na kuainisha juhudi zinazofanywa na benki hiyo katika kutekeleza mipango ya maendeleo ya Taifa alielezea changamoto mbalimbali zinazoikabili benki hiyo. Changamoto hizo ni pamoja na udogo wa mtaji, uhitaji wa kuwepo kwa fedha za kuandaa miradi, taratibu ndefu za upatikanaji wa vibali vya kukopa kwa taasisi za Serikali na uwepo wa mikopo chechefu.
 
Waziri Mpango pia aliongelea changamoto zinazo ikabili benki hiyo ikiwemo suala la mtaji ambapo alisema, “Serikali ya awamu ya tano inalifanyia kazi suala hili ili kuleta suluhisho endelevu na kuiwezesha benki hii kutimiza malengo ya kuundwa kwake”.

Pia aliisisitizia bodi kuweka mikakati madhubuti katika  kukusanya madeni, kusimamia mikopo inayotolewa  na kuhakikisha kuwa mikopo inayoidhinishwa ni kwa miradi inayo stahili na yenye uwezo wa kurejesha mikopo hiyo.

 Aidha, aliitaka benki hiyo kutokufanya kazi kwa mashinikizo yoyote kutoka kwa watu, wanasiasa, idara au taasisi yoyote; bali wazingatie sheria, kanuni na taratibu zinazoongoza tasnia ya mabenki kama zinavyoelekezwa na Benki Kuu ya Tanzania.
 
Kwa upande wake, Mwenyekiti mpya ya bodi hiyo ilioteuliwa Profesa Palamagamba John Kabudi alimuahidi Waziri kuwa watafanya kazi kwa weledi wa hali ya juu na kutekekeleza maelekezo aliyoyatoa ili kutimiza matarajio ya Serikali na waliowateua.

 Aidha, Mwenyekiti Profesa Kabudi alisema “Tutafanya jitihada ya kutafuta ufumbuzi wa changamoto mbalimbali zinazo ikabili benki yetu, Kwa yale yanayohitaji maelekezo ya ofisi yako hatutasita kuwasiliana na ofisi yako na yale yaliyoko ndani ya mamlaka yetu tutayashughulikia kulingana na taratibu za kiutendaji katika sekta husika.”

Bodi hiyo iliyozinduliwa rasmi mjini Dodoma sasa itaanza kazi zake rasmi kuhakikisha inaiendeleza na kuiimarisha Benki hiyo ya Maendeleo TIB.
 

Install Application ya JUNGUKUULEO Uweze Pata Habari Kirahisi Zaidi

xxxxxxxxxxxxx