test

Alhamisi, 27 Agosti 2015

Ukawa yang’ang’ania Jangwani



UMOJA wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) umesema utafanya mkutano wake wa ufunguzi wa kampeni za urais katika Viwanja vya Jangwani Dar es Salaam licha ya kuambiwa uwanja huo tayari ulikuwa umelipiwa. Wakati Ukawa ukisema hatua hiyo ni hujuma dhidi yake na vyama vya upinzani vinavyounda umoja huo, Halmashauri ya Manispaa Ilala imeweka wazi kilichosababisha Umoja huo kukosa viwanja hivyo katika siku hiyo. Akizungumza na mwandishi wa habari hizi juu ya malalamiko ya Chadema chini ya mwavuli wa Ukawa, Ofisa Utamaduni wa Manispaa ya Ilala, Claud Mpelembwe, alisema maombi ya kutumia uwanja huo yaliyowasilishwa na chama hicho Jumatatu wiki hii, hayakufanikiwa kutokana na kukuta uwanja huo ukiwa umelipiwa na chama kingine. Mpelembwe alieleza kusikitishwa na kitendo cha Chadema kusambaza nakala ya barua waliyoiandikia, kwenye mitandao na kutoa picha mbaya kwamba wamezuiliwa kufanya uzinduzi wao. “Kwanza tumesikitika sana, Manispaa na hata mimi binafsi, nimehuzunishwa na hawa Chadema ni wateja wetu wazuri, tunafanya kazi nao nyingi tu na hata wakati wa kuunda Ukawa walikuja kuulizia nafasi kwa tarehe walizotaka kufanyia mkutano wao Jangwani na walipata kwa kuwa hakuna mtu mwingine aliyeulipia,” alisema Mpelembwa. Aliongeza, “… sasa wenzao Chama Cha Mapinduzi (CCM), walishaulipia uwanja huo kwa tarehe hiyo, wao Chadema walipaswa baada ya majibu ya barua yetu, wangerudi kuomba au kuulizia tarehe zilizo wazi”. Alisema, awali Chadema walipeleka maombi ya kuzindua kampeni zao wizarani wakiomba kutumia Uwanja wa Taifa, maombi ambayo yalikataliwa kwa sababu zilizotajwa na kwamba wenzao, walipeleka maombi yao mapema kwa manispaa kuomba matumizi ya uwanja huo. Alisema Agosti 21, mwaka huu, CCM waliuliza uwepo wa nafasi ya kutumia uwanja wa Jangwani na ndipo walipeleka maombi kuomba kuutumia kwa maandalizi ya kuzindua kampeni zao kuanzia Agosti 21 hadi 23. “Hakuna asiyejua utaratibu wa matumizi ya viwanja vya wazi na hata kumbi za shehere au mikutano, unauliza uwepo wa nafasi kwanza kwa tarehe utakazo kama ziko wazi, ndipo unafanya malipo na kuwekewa ukumbi,”alisema Mpelembwa. Alisema CCM baada ya kulipia ukumbi huo kwa tarehe tajwa, waliuliza pia kama ipo nafasi katika uwanja huo kwa Agosti 28 hadi 30 na pia Oktoba 22 hadi 24 mwaka huu, wakajibiwa kuwa zipo nao wakalipia. “Sasa Chadema wao walileta maombi Agosti 24, na tuliwajibu uwanja umelipiwa na mtu mwingine, na tuliwashauri watafute eneo jingine na kwamba wanaweza kuutumia uwanja huo kuanzia Septemba mosi (wiki ijayo) hadi Oktoba 21, kwa sababu hakuna aliyeulipia,” alisema Mpelembwa. Ofisa huyo wa manispaa alisisitiza kwamba, baada ya wao kujibiwa hivyo, walipaswa kurudi kwa Mkurugenzi wa Manispaa kuomba tarehe nyingine jambo ambalo hawakufanya; badala yake, wamekwenda kusambaza barua hiyo kwenye vyombo vya habari na mitandao ya kijamii. “Nilishangazwa sana, baada ya kuona barua hiyo kwenye mitandao ya kijamii, na mimi ndiye ninayesimamia viwanja hivyo na huwa ninafanya kazi na Chadema, sasa walipaswa kurudi kwetu kuulizia tarehe nyingine, ila hawakufanya hivyo,” alilalamika Mpelembwa. Alitaka umma kuelewa utaratibu wa matumizi ya maeneo ya wazi kwamba yanatolewa baada ya maombi ya tarehe husika kukubaliwa iwapo hakuna mtu mwingine aliyeomba awali kutumia eneo hilo. Ukawa walalama Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mwenyekiti mwenza wa umoja unaoundwa na vyama vya upinzani- Ukawa, James Mbatia, alisisitiza kwamba mkutano wao utafanyika kama ulivyopangwa. Hata hivyo hakueleza ni wapi utafanyikia. Mbatia alisema suala hilo (la kukosa uwanja), wamemwachia Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji Damian Lubuva kwa kuwa yeye ndiye mwamuzi na si mamlaka nyingine. Alisema endapo Mwenyekiti huyo wa NEC hatachukua hatua, wataendelea na mambo yao kwa mujibu wa ratiba zao kwa kuwa ni haki yao kisheria. Alisema hawaoni sababu ya kumfuata kiongozi yeyote kwa ajili ya kuomba kibali kwa kuwa hawana imani kutokana na tofauti zao za itikadi za kisiasa. “Sisi sio wakimbizi ndani ya nchi Tanzania. Sisi ni raia halali wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Sisi tuna haki zote za kufanya kampeni hapa kwa misingi ya taratibu na sheria na ndio tukasema hatutakubali lazima kampeni zetu ziendelee hatutazuiliwa na mtu yeyote ni haki yetu,” alisema Mbatia. Aidha aliwataka wafuasi wa vyama hivyo na wananchi kwa ujumla kuwa wavumilivu katika kipindi hiki ambacho wanaendelea kutafuta ufumbuzi wa suala hili . Aliwataka kutokuwa na jazba waangalie mustakabali wa nchi kwani vyama vya siasa vinaweza kusambaratika muda wowote lakini nchi ya Tanzania itaendelea kubaki palepale. Habari hii imeandikwa na Ikunda Eric, Fadhil Akida.

Install Application ya JUNGUKUULEO Uweze Pata Habari Kirahisi Zaidi

xxxxxxxxxxxxx

0 comments:

Chapisha Maoni