Katika
siku za karibuni baadhi ya vyombo vya habari na mitandao ya kijamii
imechapisha taarifa zinazomhusisha Mke wa Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne
Mhe. Mama Salma Kikwete na Taasisi anayoiongoza ya Wanawake na Maendeleo
(WAMA) kwamba ameshindwa kulipia kodi mizigo mikubwa iliyoiingiza
nchini na hivyo kuwa hatarini kupigwa mnada.
Taarifa
hizo zimemhusisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John
Pombe Magufuli kuwa anahusika kuzuia mizigo hiyo bandarini mpaka hapo
itakapolipiwa kodi.
Tunapenda
kuutarifu umma kuwa taarifa hizo sio kweli na ni uzushi, kwani Rais
Magufuli hajawahi kuzuia wala kuagiza kuzuiwa kwa mizigo ya Mama Salma
Kikwete.
Rais
Magufuli amesikitishwa sana na uzushi huo unaofanywa kwa lengo la
kumchafua Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete na
familia yake na amewataka waandishi wa habari na vyombo vya habari
nchini kuacha kuandika na kuchapisha taarifa za uzushi na badala yake
vizingatie weledi na kufuata sheria.
“Nimesikitishwa
sana na uzushi unaofanywa dhidi ya Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho
Kikwete na Mke wake Mama Salma Kikwete, tafadhali wale mnaotengeneza
uzushi huu acheni mara moja na muacheni Rais Mstaafu Kikwete apumzike.
“Rais
Mstaafu Kikwete amefanya kazi kubwa ya kulitumikia Taifa hili,
amestaafu anapumzika, narudia muacheni apumzike, Serikali haitaendelea
kuvumilia uzushi na uchonganishi huu unaofanywa kwa makusudi ili
kuwachafua viongozi wastaafu” ameonya Rais Magufuli.
Taarifa
hii ni kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Dar es
Salaam,Gerson Msigwa kwa taarifa yake aliyoituma mchana wa jana 4 Desemba
kwa vyombo vya habari.